National News

TEMESA WATAKIWA KUIMARISHA MFUMO WA KUWAFIKIA WADAU

Tarehe: 25 Oct, 2023


Wakala wa Ufundi na Umeme nchini (TEMESA) wametakiwa kuimarisha mfumo wa kuwafikia wadau wao badala ya kusubiri kufuatwa katika maeneo yao ya kutolea huduma.

Ushauri huo umetolewa na Mkuu wa Mkoa wa Kigoma Kamishna Jenerali Mstaafu wa
Jeshi la Zimamoto na Uokojaji Thobias Andengenye alipozungumza wakati akifungua kikao cha wadau wa wakala huyo kilichofanyika Leo Oktoba 24, 2023 mjini Kigoma.

Amesema umefika wakati  TEMESA wanatakiwa kuanza kuwafuata wateja wao maeneo walipo na kuwapatia huduma, jambo litakaloongeza kasi ya utoaji huduma kwa Taasisi, Idara na Wakala wa Serikali.

Aidha Mkuu wa Mkoa amewataka wadau  wote wanaohudumiwa na wakala huyo kulipia huduma wanazopatiwa kwa wakati  ili taasisi hiyo iweze kujiendesha kwa Tija.

"Wasimamizi wa vyombo vya usafiri hakikisheni vinapelekwa kwenye matengenezo kwa wakati  kwani mnapovipeleka kwa kuchelewa mnasabaisha kuongezeka kwa gharama za matengenezo" amesisitiza Andengenye.

Aidha ameutaka uongozi wa TEMESA kutumia fursa ya maboresho makubwa  yanayofanywa na serikali ya Awamu ya Sita ndani ya taasisi hiyo kuimarisha utoaji Huduma kwa wadau wao.
..........................
Tufuatilie zaidi kupitia
#instagram @mainfmtanzania
#facebook @mainfmtanzania
#twitter @mainfmtanzania

  • © Copyright - 2024
  • All rights reserved by - MainFm
  • Developed by - Mainfintech Lab