International News

UHAMIAJI GAMBIA WATAMBULISHA SARE MAALUMU KWA MAAFISA WAJAWAZITO

Tarehe: 07 Aug, 2026


Idara ya Uhamiaji nchini Gambia (GID) imetambulisha rasmi sare mpya maalum za uzazi kwa ajili ya maafisa wake wanawake wajawazito, hatua inayolenga kuwawezesha kutekeleza majukumu yao kwa urahisi na faraja zaidi wakati wa ujauzito.


Sare hizo zimeundwa kwa kuzingatia mahitaji ya maafisa wajawazito, huku zikilenga kuimarisha ustawi wao, heshima na mazingira rafiki ya kazi wakati wanapoendelea kutekeleza majukumu yao ya kikazi.

Kwa mujibu wa hatua hiyo, uamuzi wa kuanzisha sare hizo unaelezwa kuwa sehemu ya juhudi za Idara ya Uhamiaji kuboresha maslahi ya wafanyakazi wake wa kike na kuhakikisha wanapata mazingira bora na yenye msaada katika kipindi cha ujauzito.

Hatua hiyo imepokelewa kwa mtazamo chanya na wengi, wakieleza kuwa ni ishara ya maendeleo katika kujenga mazingira ya kazi yenye ujumuisho, heshima na usawa, hususan kwa maafisa wanawake wanaotarajia kuwa kina mama.